Bila shaka, janga la Covid-19 limekuwa jambo la kawaida na sivyo kuogopewa kama pale awali. Corona ni familia ya virusi vinavyosababisha ugonjwa wa mafua, homa na kuendelea kuwa kali inaposababisha matatizo ya kupumua. Ni mripuko uliogunduliwa mwaka wa 2019.
Ujio wa Corona umebadilisha mambo mengi katika maisha yetu. Kwa mfano, namna tunavyosalimiana na pia tunavyojumuika na wenzetu hadharani. Janga hili limewaathiri waja pakubwa sana, hususan vijana. Kwanza kabisa, kuja kwa Corona kulisababisha wasiwasi kwa namna unavyosambaa haraka na kuua. Kwasababu hii, serikali ililazimika kufunga vyuo ili kuokoa maisha ya vijana. Ikafikia kufunga mipaka ya miji iliyoathirika sana na kampuni nyingi kufungwa. Hatua hii ilichangia ukosefu wa ajira kwa vijana katika sekta mbalimbali. Hali zikawa ngumu. Ukosefu wa ajira kwa njia moja au nyengine imesababisha ongezeko la uhalifu mitaani.
Alhasili, kampuni nyingi zimepunguza watu kwaajili ya Corona walakin sio wote wanaokosa ajira huingia kwenye uhalifu. Wapo wenye nidhamu ambao hutafuta mbinu aula za halali. Kuna wale wanaokosa kabisa kukidhi hata mahitaji ya kimsingi na ndipo dhiki zinapowasonga. Huzuni na hatimaye kupata unyogovu. Unyogovu pia huwezwa kusababishwa na upweke wa kukosa kutangamana na wenzao. Hali hii humaliza nguvu katika utendakazi na pia fikra zao. Unyogovu hueza kufanya kijana akajiua. Baadhi wanaojipata hapa hukata tamaa na kutokea kuingia kwenye mihadharati. Mihadharati hunyonya afya zao, huzipoteza ndoto zao, huziua aila zao na kusababisha uhalifu kuzidi.
Waambi huamba, mgala muue na haki mpe. Minghairi ya maafa maovu mna mazuri pia yanayotokana na janga hili. Naam, wako vijana wanaofaidi kwenye ajira kama vile biashara za barakoa na vieuzi. Mna ajira zilizotolewa na idhara ya afya ikiwa ni njia mojawapo katika mikakati ya kupambana na Corona. Ukosefu wa kazi, kumewafanya vijana kuzingatia kazi za mkono na za ubunifu kama vile kuandika. Hii imeboresha ujuzi wa vijana.
Ikhilasi, usafi umedumishwa. Tumekuwa tukiosha mikono yetu kila mara kwa kutumia vitakasa. Makaazi, mitaa na majumba yamekuwa yakisafishwa mara kwa mara ili kuviua virusi hivi. Isitoshe, kipindi hichi cha Corona, kumekuwa na ongezeko kubwa kwa vijana katika utumiaji wa teknolojia. Mikutano, warsha, mafunzo na kadhalika zinafanywa mitandaoni. Hii imerahisisha mambo mengi pamoja na kuepuka uwezekano wa kupata maradhi haya.
Hatimaye, naweza kusema kuwa janga hili ni kama msumeno, hukata mbele na nyuma. Tukumbuke kuwa maisha yanapokuwa jasiri inatulazimu tujasirike. Inatupasa kumuweka MwenyeziMungu mbele na kumuomba atuepushe na maradhi haya. Nasi vijana tunafaa kushirikiana, kuelimishana na kusaidiana, katika kipindi hichi cha janga la Corona, ikirari, nguzo moja hiajengi nyumba.